- Viongozi hao wa Chadema walikamatwa Julai 15 kwa kosa la kufanya maandamano bila kibali na kwa sasa jalada lao lipo kwa wakili wa Serikali mfawidhi mkoa wa Ruvuma.
Songea. Viongozi tisa wa Chadema akiwamo Katibu Mkuu Taifa wa chama hicho, DkVicent Mashinji wameripoti kwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma leo saa 4 asubuhi kama walivyotakiwa kufanya.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake leo Jumanne, Julai 18, kamanda huyo, Gemini Mushi amesema viongozi hao wameripoti ofisini kwake leo asubuhi na mpaka sasa wapo hapo wakisubiri jalada la kesi yao.
Imeelezwa kuwa jalada lao lipo kwa wakili wa serikali mfawidhi mkoa wa Ruvuma. Viongozi hao walikamatwa na Polisi Julai 15, kwa madai ya kufanya maandamano bila kibali.
Pamoja na Dk Mashinji, wengine waliokamatwa ni mbunge wa Ndanda, Cecil Mwambe, Philberth Ngatunga ambaye ni Katibu wa Chadema Kanda ya Kusini, Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Ruvuma, Erineus Ngatura na Katibu wa Chadema mkoa wa Ruvuma, Delphin Gazia.
Wengine ni Zubeda Sakuru, mbunge viti maalum mkoa wa Ruvuma (Chadema), Sang’uda Moses, mkuu wa Oganaizesheni na Mafunzo (Chadema), Curthberth Ngwata Mwenyekiti Wilaya ya Nyasa pamoja na Charles Makunguru ambaye ni Katibu Mwenezi Wilaya ya Nyasa.


0 comments :
Post a Comment