Tanzania Yaanza Kusaka Amani Burudi......Waziri Mahiga Ateta Na Rais Nkurunziza Kwa Masaa Mawili


WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk Augustine Mahiga, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Pierre Nkurunziza wa Jamhuri ya Burundi, kwenye Ikulu yake jijini Bujumbura.

Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, iliyotumwa jana kwa vyombo vya habari, ilifafanua kwamba hatua hiyo ya Dk Mahiga, ni utekelezaji wa maagizo ya Rais John Magufuli.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Rais Magufuli ambaye ndiye Mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashiriki, ameamua kutafuta suluhu ya kisiasa ya migogoro iliyojitokeza baina ya Serikali na vikundi vinavyo hatarisha amani nchini humo.

Imeelezwa kuwa kwenye mazungumzo hayo yaliyodumu takriban saa mbili, Dk Mahiga alimueleza Rais Nkurunziza azma ya Rais Magufuli kuamsha mazungumzo ya kisiasa ya kuleta amani.

Dk Mahiga pia alieleza kwamba tayari msuluhishi aliyeteuliwa na Jumuiya hiyo, Rais Yoweri Museveni, ameanza maandalizi ya uzinduzi wa mazungumzo hayo, yatakayofanyika Entebe, Uganda wiki ijayo Desemba 28 mwaka huu.

Waziri Mahiga pia alieleza maoni yake kuhusu hali ya utulivu aliyoiona kwa kipindi cha takriban saa 24 alizokuwa jijini Bujumbura na kwamba hakusikia sauti za milipuko wala silaha zozote.

Baada ya mazungumzo hayo, taarifa hiyo imeeleza kuwa Rais Nkurunziza alimshukuru Rais Magufuli na kumhakikishia ushiriki wa Burundi, akieleza kuwa mazungumzo ya Entebe yatasaidia kuleta amani na mshikamano baina ya wananchi wa Burundi.

Hata hivyo, taarifa hiyo imeeleza kuwa Rais Nkurunziza alisisitiza kuwa ili mazungumzo hayo yawe na tija, ni lazima yawe na muendelezo wa ndani, ambao yeye na Serikali yake wamekwisha yaanza.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Rais Nkurunziza alisema ni matumaini yake kuwa makundi yote nchini humo, wataungana kwenye mazungumzo hayo yatakayojumuisha asasi za kiraia, kidini, vyama vya siasa na makundi mengine, ili kujadili mustakabali wa Taifa lao kwa pamoja.

Pamoja na kuridhia ushiriki wa Burundi kwenye mchakato huo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, taarifa hiyo imeeleza kuwa Rais Nkurunziza alieleza kuwa yeye na Serikali yake wako tayari kushirikiana na Umoja wa Afrika (AU) na Umoja wa Mataifa (UN) kutathmini hali ya usalama nchini mwake.

Hivi karibuni Baraza la Amani na Usalama la AU, lilitangaza azma ya kupeleka vikosi vya askari 5,000 nchini Burundi, kutokana na kuonekana viashiria vya mauaji ya kimbari kama yale yaliyofanyika nchini Rwanda miaka ya tisini.

Lakini taarifa hiyo imeeleza kuwa, Rais Nkurunziza alisema uamuzi huo wa AU, umewashitua wao serikalini na hata wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi, waliofikia hatua ya kuhoji sababu za umoja huo kupeleka jeshi kubwa nchini humo.

“Burundi imekuwa ikishirikiana na Umoja wa Afrika (AU) kwenye ulinzi wa amani ambapo ina vikosi vya askari zaidi ya elfu sita nchini Somalia na Afrika ya Kati,” amekaririwa Rais Nkurunziza akisema.

Naye Spika wa Bunge la Burundi, Paschal Nyabenda alieleza kusikitishwa kwake na uamuzi huo wa AU, ambapo alimweleza Dk Mahiga kuwa misingi ya kukataa ukabila imeainishwa kwenye katiba ya nchi hiyo na makubaliano ya Arusha.

Spika huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama Tawala cha CNDD-FDD nchini humo, alisema kuwa Katiba ya nchi hiyo, inalazimisha taasisi zote ziwe na uwakilishi na pengine uwiano sawa kati ya Wahutu na Watusi.

Akielezea muundo wa Bunge lake, Taarifa hiyo imeeleza kuwa Spika huyo alisema Bunge hilo lina asilimia 60 kwa 40 ya uwakilishi wa Wahutu na Watusi. Spika Nyabenda alisema kuwa Makamu wa Kwanza wa Spika, Agathon Rwasa anatoka kwenye kabila la Wahutu na Makamu wa Pili wa Spika, Edouard Nduwimana anatokea kwenye kabila la Watusi.

Aidha, Naibu Spika wa Kwanza wa Bunge hilo, Agathon Rwasa ambaye pia alishiriki kwenye mazungumzo hayo, alisema kuwa wakati umefika sasa kwa Burundi kuangalia mbele na kwa manufaa na maendeleo ya vizazi vijavyo na kusifu maendeleo aliyoyashuhudia nchini Tanzania ambapo alisisitiza yamekuwepo kutokana na amani nchini humo.

Akiwa nchini Burundi, Dk Mahiga na ujumbe wake walikutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa Wizara ya Usalama wa Raia na Mambo ya Ndani, ambapo alipokea taarifa ya Waziri Alain Guillaume Bunyoni, kuhusu hali ya usalama nchini humo tangu Rais Nkurunziza alipochaguliwa na chama chake kugombea tena nafasi ya urais Aprili mwaka huu.

Kwa upande wake, Waziri Mahiga alisifia jitihada zilizowekwa na Wizara hiyo, hususan kwenye upande wa ulinzi wa raia na mali zao na kusisitiza umuhimu wa Wizara hiyo na Serikali nzima, kuwaelezea wananchi na jumuiya za kimataifa jitihada za Serikali kuleta amani nchini humo.

Katika ziara hiyo ya siku mbili, Waziri Mahiga pia alifanya mazungumzo na Dk Crispus Kiyonga, Waziri wa Ulinzi wa Uganda, ambaye ameanza maandalizi ya mazungumzo ya amani chini ya uenyekiti wa Rais Museveni wa Uganda.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment