Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Marekani linaloshughulikia masuala ya kijeshi 
barani Afrika, Meja Jenerali Darrly Williams, amemtunuku mkuu wa majeshi
 ya vikosi vya nchi kavu Tanzania Meja Jenerali James Mwakibolwa nishani
 ya ulipuaji bora wa mizinga nchini. 
Nishani hiyo ambayo imekuwa
 ikitolewa na Rais wa Marekani, alitunukiwa Meja Jenerali Mwakibolwa 
baada ya kuwa mstari wa mbele kurudisha amani kwenye nchi zinazokabiliwa
 na vita barani Afrika. 
Akizungumza wakati wa kufunga mkutano wa
 wakuu makamandi wa vikosi vya nchi kavu barani Afrika, uliofanyika 
mkoani Arusha, Jenerali Williams alisema jeshi la Marekani barani Afrika, 
linamtambua Mwakibolwa kuwa mchapa kazi bora. 
“Mwakibolwa ni mtaalamu 
sana kwenye masuala ya mizinga, hata tulipokwenda kwenye mafunzo ya 
kijeshi katika kambi ya Monduli, tumeona umahiri wake na tuzo hii 
anastahili kwa kuwa anafanya vizuri.
 “Jeshi la Tanzania limekuwa mstari 
wa mbele kutoa kikundi cha M23 kwenye nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya
 Congo (DRC) na yote hayo ni kutokana na uchapakazi wa Jenerali 
Mwakibolwa,” alisema Jenerali Williams. 
Akitoa maoni yake kuhusu
 tuzo hiyo, Jenerali Mwakibolwa aliahidi kuhakikisha Jeshi la Tanzania 
linakuwa imara zadi barani Afrika. 
Alisema Tanzania inazingatia masuala ya kijinsia katika jeshi hilo na sasa asilimia 25 ya wanajeshi ni wanawake. 
“Jeshi
 la Tanzania tuna wanawake wenye vyeo vikubwa na wako ambao tumewapa 
kazi kwenye idara mbalimbali. Tunaamini mwanamke anaweza,” alisema 
Jenerali Mwakibolwa. 
Kuhusu maazimio ya mkutano huo, alisema 
wanaangalia namna ya kutoa mafunzo ya kupambana na ugaidi wa baadhi ya 
wanajeshi wa Afrika. 
Naibu Katibu wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi 
la Tanzania, Immaculate Ngwale alisema mkutano huo umekuwa na faida kwa 
kuwajengea uimara askari wake. 



Blogger Comment
Facebook Comment