WAJUMBE wa Baraza la Wawakilishi wamekaa kimya kwa muda wa dakika 
moja kumkumbuka aliyekuwa Rais wa awamu ya pili ya Zanzibar, Aboud Jumbe
 Mwinyi aliyefariki mwezi uliopita ambaye alikuwa muasisi na mwanzilishi
 wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, ambacho ni chombo cha kutunga 
sheria.
Spika wa Baraza la Wawakilishi, Zubeir Ali Maulid alisoma wasifu wa 
Mzee Jumbe na kusema atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika kukuza 
na kuimarisha demokrasia, ikiwemo kuanza kwa harakati za kutungwa kwa 
katiba ya kwanza ya Zanzibar ya mwaka 1979 pamoja na kuanzishwa kwa 
Baraza la Wawakilishi katika mwaka 1980.
“Huo ndiyo mchango mkubwa wa Jumbe katika harakati za demokrasia 
Zanzibar ambayo ilifanya kuanzishwa kwa Baraza la Wawakilishi ambapo 
yeye binafsi aliita ndiyo ngome ya wananchi,” alisema.
Maulid alisema mchango mkubwa wa Jumbe ni kuchangia kuzaliwa kwa 
Chama Cha Mapinduzi(CCM) mwaka 1977 baada ya kuvunjwa kwa vyama vya Tanu
 na ASP na kuzaliwa chama kipya ambacho kimefanikiwa kushika hatamu ya 
uongozi hadi leo.
Jumbe alikuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi 
pamoja na Makamu wa rais wa Jamhuri ya Muungano kuanzia mwaka 1972 hadi 
mwaka 1984 wakati alipolazimika kujiuzulu nyadhifa zote kwa sababu za 
kuchafuka kwa hali ya kisiasa Zanzibar.
Chanzo :swahiba  media


0 comments :
Post a Comment