Msemaji
wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Christopher Ole Sendeka amemtaka Rais John
Pombe Magufuli kukagua akaunti za kamati za bunge na viongozi wake
hususani zile zinazosimamia mashirika na taasisi za umma zilizotajwa
kuwa na ufisadi.
Ole
Sendeka ametoa wito huo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari
katika makao makuu ya CCM yaliyopo Lumumba, jijini Dar es Salaam.
Pia
amemsisitiza Rais Magufuli kuendelea kukagua taasisi, mashirika ya umma
pamoja na wizara ili kubaini wanaotumia fedha za serikali kinyume cha
sheria.
“Serikali
iendelee kukagua mashirika na wizara ili waliotumia fedha kinyume cha
sheria na taratibu wachukuliwe hatua za kisheria kwa kupelekwa
mahakamani,” amesema.
Ameongeza
kuwa “Wakati umefika kwa serikali ya CCM kutoshughulikia maafisa
masuhuli wa mashirika na taasisi hizo pekee, bali waangalie na akaunti
za viongozi wa kamati za bunge ambao walikuwa wanasimamia taasisi na
mashirika yaliyokutwa na ufisadi,” amesema.
Licha
ya hayo, Ole Sendeka amedai kuwa kuna baadhi ya matajiri wanaokwepa
kulipa kodi huutumia utajiri wao kushawishi baadhi ya vijana kuikejeli
serikali pamoja na kuvishawishi vyombo vya habari vya ndani na nje ya
nchi kuandika makala zenye lengo la kuichafua serikali.
“Tunajua
kwamba hawana ujasiri wa kusimama na kusema wanalazimishwa kulipa kodi,
baadhi yao wametubu na kufuata kanuni na sheria za ulipaji kodi, lakini
wengine wanatumia ukwasi wao katika kushawishi baadhi yavyombo vya
habari vya nje na ndani ya nchi kuandika makala za kuikejeli na
kuichafua serikali,
“Kumekuwepo
na usambazaji wa taarifa za upotoshaji zinazotolewa na baadhi ya
wanasiasa kupitia katika baadhi ya vyombo vya habari vya ndani na nje ya
nchi, makala hizo zinalenga kukejeli, dhihaki, kubeza na kuikatisha
tamaa serikali ili ishindwe kutekeleza majukumu yake,” amesema.
Amesema
licha ya kejeli hizo, serikali itaendelea kuwa imara na kwamba utendaji
kazi wake hautafutika katika mioyo ya wananchi kwa sababu ya kelele za
baadhi ya watu.
“Serikali ya Magufuli haina gia ya kurudi nyuma itaendelea kusonga mbele,” amesema.
Hata
hivyo, Ole Sendeka amesema CCM inatarajia kutoa taarifa za mafanikio na
utekelezaji wa ilani yake katika kipindi cha mwaka mmoja kabla ya
Novemba 5, 2016.


0 comments :
Post a Comment