Madiwani wanawake wa vyama mbalimbali vya siasa katika Mkoa wa Dar es Salaam wamesema suala la kubadili mtazamo katika ushirikishwaji wa wanawake kwenye maendeleo ni la msingi na linapaswa kutekelezwa kuanzia ngazi za chini.
Wakizungumza katika warsha ya siku tatu ya Uongozi wa Kijinsia iliyoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP Mtandao), madiwani hao wamesema haki za wanawake bado zinakandamizwa katika jamii huku vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vikishika kasi.

Spika Mstaafu na Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Anne Makinda akiwahamasisha Madiwani wanawake wa Jiji la Dar es Salaam walioudhuria mafunzo ya uongozi, jinsia na bajeti yenye mlengo wa kijinsia pamoja na kutoa uzoefu wake kwenye maswala ya uongozi kwa wanawake hasa ngazi za juu leo kwenye ukumbi wa TGNP Mtandano jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mafunzo ya siku tatu Spika Mstaafu na Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Anne Makinda amesema wanawake wanapaswa kuungana kwa pamoja wanapokuwa wanapigania haki zao za msingi. Amewasisitiza kuachana na masuala ya vyama kwenye jambo linalowahusu wanawake wote. Wakifanya hivyo wataweza kupunguza tabaka kubwa kwenye utawala na hata kwenye uzalishaji mali.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Bi Lilian Liundi amesema watoto wa kike wanakosa vipindi vya masomo kutokana na ukosefu wa elimu ya kujihifadhi hasa wanapokuwa katika hedhi.
“Elimu ya hedhi bado duni sana, hasa vijijini kwa sababu watoto wengi wa kike wanapokuwa katika hedhi huhisi kwamba ni wagonjwa, hivyo hushindwa kuhudhuria vipindi ipasavyo lazima elimu hii itolewe kwa jamii ili kuwawezesha watoto hawa wapate elimu kama ilivyo kwa wale wa kiume,” alisema Lilian Liundi.Facebook