Nkupamah media:
Mwenyekiti
 wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji mstaafu Damian Lubuva, amesema
 mchakato wa Kura ya Maoni ya Katiba mpya umeanza baada ya kumalizika 
kwa Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25, mwaka jana.
Kauli
 hiyo ya Jaji Lubuva imekuja wakati wadau wa siasa nchini wakimtaka Rais
 Dk. John Magufuli, kutoendelea na Kura ya maoni badala yake mchakato wa
 Katiba mpya urudi nyuma baadhi ya mambo yaliyo kwenye Katiba 
iliyopendekezwa yarekebishwe.
Itakumbukwa
 kuwa mchakato wa Katiba mpya uliingia dosari baada ya baadhi ya 
viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kupinga mfumo wa Serikali Tatu 
uliokuwa umependekezwa na Tume ya Jaji mstaafu Joseph Warioba, 
iliyokusanya maoni nchi nzima na matokeo yake kuzaa kundi lililojiita 
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
“Tulikuwa
 tunangoja tumalize uchaguzi, kama vile ambavyo Mnyamwezi anavyobeba 
mzigo, unamaliza mmoja unakwenda kwa mwingine. Sasa tumemaliza (uchaguzi
 mkuu), tunakwenda kwa lingine (Kura ya Maoni),” alisema Jaji Lubuva.
Aliongeza: “Tunaliangalia
 na kama Tume tutakuja kuwajulisha wananchi hali ikoje, tuliahirisha 
(Kura ya Maoni) ili tumalize hili (uchaguzi mkuu).” alisema Jaji Lubuva na kuongeza.
“Hili
 ni suala linalohitaji mambo ya bajeti kubwa na ndiyo tumetoka kwenye 
uchaguzi na serikali ndiyo inaanza, kwa hiyo ni suala ambalo 
tunaliangalia na baadaye wananchi watajulishwa,” alisema Jaji mstaafu Lubuva.
Alipoulizwa kuhusu makadirio ya bajeti ya kuendesha kura hiyo ya maoni, Lubuva alisema: “Hilo niulize siku nyingine, sina zaidi ya hapo kwa leo.”
Rais
 Magufuli alipokuwa akihutubia Bunge la 11 siku ya kulizindua Novemba 
20, mwaka jana, alisema serikali yake imepokea kiporo cha mchakato wa 
Katiba ambao haukukamilika katika awamu iliyomtangulia kutokana na 
kutokukamilika kwa wakati kwa uandikishaji wapiga kura. 
“Napenda
 kuwahakikishia kuwa tunatambua na kuthamini kazi kubwa ya kizalendo 
iliyofanywa na wananchi walioshiriki hatua ya awali ya ukusanyaji wa 
maoni kuhusu Katiba mpya, Tume ya Marekebisho ya Katiba na Bunge la 
Katiba lililotupatia Katiba Inayopendekezwa. Tutatekeleza wajibu wetu 
kama ulivyoainishwa katika Sheria ya Marekebisho ya Katiba,” alisema Rais Magufuli.  
Mbali
 na muundo wa serikali tatu, baadhi ya mambo ambayo Ukawa walitaka yawe 
kwenye Katiba mpya ni mamlaka ya Rais kupunguzwa, ushindi wa Rais uwe 
zaidi ya asilimia 50, Tume huru ya Uchaguzi, matokeo ya Rais kupingwa 
mahakamani, kuwe na mgombea binafsi, mawaziri wasitokane na wabunge, na 
muundo mpya wa Bunge la Muungano.



0 comments :
Post a Comment