Baada
ya Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF) Profesa Ibrahim Lipumba
kukituhumu chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuwa kinaivuruga
chama chake. Chadema imekanusha madai hayo na kudai kuwa Lipumba ndiye
msaliti wa harakati za kutetea masilahi ya demokrasia nchini na Umoja wa
Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Mwenyekiti
wa Chadema Taifa Freeman Mbowe leo amesema kuwa chama hicho sambamba na
viongozi pamoja na wafuasi wake hawamtambui Lipumba kuwa ni Mwenyekiti
wa CUF na kwamba chama hicho hakitatoa ushirikiano kwake na hata kwa
wafuasi wake.
“Kamati
maalumu ya kamati kuu imepokea taarifa ya mgogoro unaondelea ndani ya
CUF unaomhusisha aliyekuwa mwenyekiti Taifa wa chama hicho Profesa
Ibrahim Lipumba, pia kamati inatambua kuwa mgogoro huu unachochewa na
utawala wa kiimla wa Rais Magufuli kwa kumtumia Msajili wa Vyama vya
Siasa Jaji Francis Mutungi, ” amesema.
“Kamati
inavielekeza vyombo vyote vya chama chetu, viongozi wa ngazi, wanachama
na wafuasi wa chama chetu na wapenda demokrasia wote nchini kumuangalia
Lipumba kama msaliti wa harakati za kudai haki nchini na kutokumpa yeye
na wafuasi wake ushirikiano wa aina yoyote ,” amesema.
Katika
hatua nyingine viongozi wa vyama vinavyounda umoja huo, wameandaa
mkutano utakao fanyika kesho jijini Dar es Salaam wenye lengo la
kumjadili Lipumba.
Mgogoro
wa CUF unaondelea sasa huenda ukapelekea chama hicho kujiondoa katika
UKAWA na au kutotekeleza baadhi ya makubaliano ya umoja huo.
Kwa
sababu, leo Lipumba ambaye ni mwenyekiti wa chama hicho, ametamka
hadharani kuwa CUF iko tayari kusimamisha mgombea wake katika uchaguzi
mkuu ujao na kudai kuwa umoja huo hauna mamlaka kikatiba ya kusimamisha
mgombea kwa niaba ya vyama vyote vinavyounda umoja huo.
Moja
ya makubaliano ya Ukawa ni kuwa unasimamisha mgombea mmoja wa urais
kutoka chama kimoja, atakayeungwa mkono na vyama vinavyounda umoja huo,
jambo ambalo linaonekana kutoungwa mkono na Lipumba aliyekiri kuwa chama
chake hapo baadae kitasimamisha mgombea wake.
Licha
ya kauli hiyo ya Lipumba kudhihirisha kuwa haungi mkono UKAWA, pia
ameutuhumu umoja huo kuwa umepotea kisiasa na kwamba vyama vinavyounda
umoja huo vimeshindwa tekeleza adhma yake ya kupambana na rushwa,
ufisadi na kuitetea rasimu ya katiba ya jaji Joseph Warioba baada ya
kumpokea Edward Lowassa aliyemtuhumu kuwa aliipinga rasimu hiyo.
Lipumba
alisema kuwa “Ukawa imepotea kisiasa baada ya kumpokea Lowassa, imeacha
kupambana na rushwa, ufisadi na badala yake Rais Magufuli ndiyo
anatekeleza na kupambana na vita hiyo.”
Ameongeza
kuwa “Lengo la Ukawa ni kuitetea rasimu ya Warioba, awali lowassa
hakuitetea na hakuiunga mkono. Wananchi waelewe kuwa Ukawa si chama cha
siasa na imesahau majukumu yake ya kupigania rasimu ya katiba ya
warioba.”
Endapo
Lipumba ataendelea na wadhifa wake huo na kuendelea na misimamo yake ya
kutokubali umoja huo kumuunga mkono Lowassa, ikiwa Ukawa itamchagua
Lowassa kugombea urais 2020, anaweza akaumegua umoja huo kutokana na
misimamo yake.


0 comments :
Post a Comment