Nchi hii si ya viongozi au wanasiasa pekee

Posted  Jumanne,Marchi18  2014  Na mwananchi
Kwa ufupi
Mnapojiita viongozi kwa maana ya uwaziri, umeya, ukuu wa mkoa, ukurugenzi wa halmashauri na vyeo vingine, hamuongozi miti na mawe, mnawaongoza watu waitwao Watanzania
.
SHARE THIS STORY

Ninapofuatilia kadhia wanazokumbana nazo Watanzania karibu kila kona ya nchi hii, nabaki nikijiuliza hivi nchi hii ni kwa ajili ya nani hasa?
Ukweli ni kuwa ndani ya nchi yao Watanzania hawana raha. Kila siku ni mateso kutoka kwa wale tuliowatarajia kuwa huenda wangekuwa watetezi wao.
Katika baadhi ya maeneo nchini, wananchi wananyang’anywa ardhi zao kwa nguvu ili kupisha wawekezaji wa kigeni watumie ardhi hiyo.
Iko haja ya kuwapasulia ukweli viongozi wetu. Hata kama mmeamua kutunyonya wananchi na kuchota asali na maziwa yote ya nchi, basi msile na kutapanya rasilimali zote. Vizazi vyenu na vyetu vitakuja kula nini?
Madini sasa yanatoweka, ardhi yenye rutuba nzuri mmejimilikisha ekari zake kwa maelfu, achilia mbali mnazowanyanganya wananchi kila siku kwa kisingizio cha uwekezaji au kulinda maeneo ya hifadhi.
Sasa mnanuwia kuwapa wageni gesi na mafuta, huku mkiwatenga na kuwaponda wazawa. Hivi nchi hii itabakiwa na nini miaka 100 ijayo?
Kama waasisi wa Taifa hili wangetapanya rasilimali enzi zao, leo mngepata kiburi cha kuwasimanga wazawa kuwa hawana uwezo wa kuwekeza katika sekta za gesi na mafuta?
Sisi wananchi hatuna shida na kula kwenu. Kuleni na msaze lakini wekeni mazingira mazuri ya kila Mtanzania kuishi japo maisha ya kawaida. Jengeni barabara ili mkipita na mashangingi yenu, sisi tupite na baiskeli au pikipiki zetu.
Iko wapi raha ya kuendesha gari la Sh200 milioni katika barabara yenye viraka na mashimo? Tuwekeeni miundombinu ya maji na umeme, ili hata msipolipa bili, sisi wanyonge tutawafidia kwa kulipishwa bei kubwa, ili Tanesco iweze kujiendesha.
Simamieni kikamilifu mifumo ya kodi ili watu wengi zaidi wakiwamo wafanyabiashara, wapangishaji wa nyumba na fremu nao walipe kodi badala ya kutegemea kodi za wafanyakazi pekee. Kodi ikiwa kubwa hamuoni kuwa nanyi mtapata fungu kubwa zaidi la kulipana mishahara, posho na kufanya ‘’matanuzi’?
Mnapojiita viongozi kwa maana ya uwaziri, umeya, ukuu wa mkoa, ukurugenzi wa halmashauri na vyeo vingine, hamuongozi miti na mawe, mnawaongoza watu waitwao Watanzania.
Hawa ndiyo wanaowafanya nyinyi mkaitwa viongozi na hatimaye kutambulika ndani na nje ya nchi. Hata kula kwenu kunatokana na wao, kwani ndiyo wanaohenyeka ili nyinyi wakubwa mtembelee mashangingi na kuishi katika majumba ya kifahari jirani na fukwe za bahari.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment