Mbarawa kutumbua majipu TBA, TTCL


WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa amesema katika kipindi cha wiki mbili atafanya `safisha safisha’ katika baadhi ya taasisi zilizo chini ya wizara yake.
Amesema hatua hiyo inatokana na kutoridhishwa na utendaji wa baadhi ya watendaji wake. Mbarawa alizitaja taasisi hizo kuwa
Wakala wa Majengo (TBA), Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa) na Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) kutokana na taasisi hizo kuhujumiwa na watendaji wake wachache.
Alitoa kauli hiyo juzi wakati akizungumza na wafanyakazi mkoani Simiyu na Shinyanga kwa nyakati tofauti kutoka taasisi na mashirika yaliyoko chini ya wizara yake kwa viongozi wa chini kufanya kazi kwa mazoea.
Kauli hiyo ilikuja baada ya waziri huyo kupokea malalamiko kutoka kwa baadhi ya wafanyakazi wa taasisi hizo, ambao walidai kutolipwa fedha za uhamisho, kutokupandishwa madaraja pamoja na wengine kufanyakazi kama vibarua kwa muda wa zaidi ya miaka mitatu.
Alisema anatambua matatizo makubwa yanayowakabili wafanyakazi kutoka Temesa, TTCL na TBA kwa kile alichoeleza kuwa viongozi wamefanya taasisi hiyo kama sehemu ya kujinufaisha wenyewe.
“Matatizo yenu siyo mageni kwangu na wala sishangai kuyasikia... lakini nawaomba ndani ya wiki moja au mbili nafanya zoezi kubwa la safisha safisha kwenye mamlaka hizi kusema ukweli nachukia sana utendaji wa taasisi hizi,” alisema Mbarawa.
Alisema Temesa wamekuwa wakipata kazi kubwa na nyingi za kutengeneza magari ya serikali, ambapo alisema amekuwa akishangazwa kusikia wakala huo hauna uwezo wa kujiendesha.
Kwa upande wa TTCL, alisema tayari amepata taarifa na anafahamu kuwepo kwa baadhi ya wafanyakazi ndani ya shirika hilo wanaolihujumu kupitia mashirika ya mawasiliano mengine ya binafsi yakiwamo ya simu za mkononi.
Kuhusu TBA, alisema kuwa kasi ya utendaji wake imekuwa hairidhishi kutokana na wakala huyo kushindwa kujiendesha licha ya kupata kazi nyingi za ujenzi kutoka serikalini.
Katika ziara hiyo iliyokuwa ya kukagua miradi mbalimbali iliyoko chini ya wizara yake ikiwemo barabara pamoja na kuzungumza na wafanyakazi wake, aliwataka watendaji kuhakikisha wanafanya kazi kwa ufanisi na ufasaha.
Alisema hatawavumilia watendaji wasio waadilifu, na wala rushwa. Alizitaka taasisi zilizo chini ya wizara hiyo, ikiwemo Tanroads kutumia kwa njia sahihi fedha za umma, ikiwa pamoja na kuhakikisha zinakusanya kodi kama inavyotakiwa kwa zile taasisi zinazojihusisha na ukusanyaji kodi.
Share on Google Plus

About Mng'atuzi blog

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment