Wazazi walalamika kuchangishwa fedha kwa wanafunzi wa darasa la awali

Wazazi na walezi wa wanafunzi  122 wa darasa la awali katika shule ya msingi Kinampundu, tarafa ya Nduguti, wilayani Mkalama wameulalamikia uongozi wa shule ya msingi Kinampundu kwa tuhuma za kuwachangisha kila mmoja shilingi 5,000/= kwa ajili ya kuandikisha wanafunzi wanaoanza masomo ya darasa la awali katika shule hiyo.
Kuchangishwa kwa kiasi hicho cha fedha kwa wazazi na walezi wa shule hiyo ni ukiukwaji wa agizo la Rais Dk.John Pombe Magufuli alilotangaza juu ya elimu bila malipo kwa wanafunzi wa kuanzia darasa la awali mpaka sekondari.
Kauli hiyo imetolewa na wazazi na walezi wa wanafunzi wa shule hiyo katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na mbunge wa jimbo la Iramba Mashariki(CCM), Allani Joseph Kiula aliyekuwa katika ziara yake ya kuwashukuru wananchi wa kata hiyo kwa kumchagua ikiwa ni pamoja na kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa kwa nguvu za wananchi katika jimbo hilo.
Mmoja wa wazazi, Pendaeli John alifafanua kwamba licha ya kiongozi mkuu wa nchi kuagiza kwamba wanafunzi wa kuanzia darasa la awali hadi sekondari watanufaika na elimu bila malipo lakini cha kushangaza agizo hilo limeendelea kupuuzwa na baadhi ya walimu wa shule hiyo huku watendaji wenye mamlaka ya kutoa maamuzi katika kata hiyo wakiwa kimya.
Aidha kwa upande wake mzazi mwingine, Cosmas Amasi aliweka wazi kwa kuzitaja sababu zinazochangia wao wadaiwe shilingi  5,000 kwa mwaka, kutokana na maelezo ya walimu wa shule hiyo sababu ya kuweka malipo ni idadi ndogo ya walimu waliopo shuleni hapo,jambo ambalo lipo ndani ya uwezo wa serikali.
“Tunaambiwa kwamba ni lazima kila mzazi au mlezi achangie shilingi elfu tano kwa mwaka kutokana na idadi ya walimu waliopo katika shule hii ni wachache hivyo ni jukumu la wazazi kuchangia ili mwalimu anayefundisha watoto hao aweze kulipwa  posho yake ya mwezi”alifafanua Amasi.
Naye Lazaro Kingu akizungumzia ujenzi wa vyumba vya maabara katika shule ya sekondari ya kata hiyo alisisitiza kwamba wananchi wa kata hiyo walichangishwa pia shilingi 65,000/= kila mmoja kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya maabara lakini tangu kuanza kwa ujenzi huo mpaka sasa jengo hilo bado halijakamilika kujengwa licha ya fedha nyingi kukusanywa na uongozi wa kata hiyo.
Hata hivyo walipotaka kuzungumzia malalamiko ya wananchi hao, Afisa Mtendaji wa kata hiyo, Richard Laizer pamoja na mwalimu mkuu wa shule hiyo, Hamisi Mbutu walikiri wananchi kuchangia kiasi hicho cha fedha lakini kwa upande wao hawakuhusika katika zoezi zima la ukusanyaji wa michango hiyo.
 Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Iramba Mashariki, Allani Joseph Kiula alisema kwamba wazazi pamoja na walezi wa shule hawana budi kutambua kwamba shule ni mali yao kwani ni kwa kiasi kikubwa sana wao wameshiriki katika ujenzi wa shule hiyo.
Alibainisha pia kwamba kutokana na ukweli huo wa ushiriki wao katika ujenzi wa shule hivyo kunapohitajika mchango wowote ule uongozi wa shule na kata kwa ujumla hawana budi kukubaliana katika vikao vya maamuzi ya pamoja na kisha kwenda kuomba kibali cha kuchangisha,ambacho mwenye mamlaka ya kutoa kibali hicho ni mkuu wa mkoa peke yake.
“Kwa kuwa shule ni mali ya wananchi,kwani hakuna anayebisha kuwa wao ni washiriki wakuu katika ujenzi wa shule hii,hivyo kunapotokea mchango wowote wa shule mnawajibika kukutana katika vikao halali na kisha kupeleka maaombi kwa mkuu wa wilaya na hatimaye kwa mkuu wa mkoa ambaye ndiye mwenye mamlaka pekee ya kuruhusu michango yeyote ile,” alisisitiza Mbunge huyo.
Na Jumbe Ismailly, Mkalama
DSCN0213Afisa elimu wilayani Mkalama (aliyesimama huku akiwa na karatasi mkononi) akifafanua jambo kuhusu suala la elimu bila malipo.
DSCN0220Mbunge wa jimbo la Iramba mashariki(CCM), Bwana Allani Kiula(wa pili kutoka kushoto) akiwa na diwani wa kata ya Ilunda, Bwana Mohamedi Imbele(wa pili kutoka kushoto) wakiwa katika mkutano wa hadhara katika Kijiji cha Kinampundu.
DSCN0226Mbunge wa jimbo la Iramba mashariki(CCM)Bwana Allani Kiula(wa kwanza kutokaa kulia) akimtambulisha afisa mtendaji wa kata ya Kinampundu kwa wananchi waliohudhuria mkutano huo.
DSCN0266Baadhi ya wanawae waliohudhuria mkutano wa mbunge na kutoa kero zao zinazowasumbua.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment