Mwenyekiti  wa CCM wilaya ya Singida, Narumba Hanje, amewashauri viongozi wa madhahebu ya dini mbalimbali kutenga muda wakati wa ibada kuliombea taifa ili liweze kuondokana na mauaji ya kikatili ya watu wasio na hatia yanayoendelea kushamiri hivi sasa kila kona ya nchi.
Hanje ametoa wito huo juzi wakati akizungumza kwenye mazishi ya aliyekuwa Afisa Mwandamizi wa Utafiti Kilimo Uyole Mbeya, Dk.Sofia Swai Mbogho, yaliyofanyika katika kijiji cha Mtinko.
Hanje ambaye amejibatiza jina la askofu wa kujitegema, alisema Tanzania hivi sasa haina salama, imekubwa na balaa kubwa la watu wasio na hatia yoyote kuuawa kikatili.
“Hali ni mbaya sana ndugu zanguni, nadhani sote tumesikia familia moja ya watu saba wameuawa kama nyoka, wapo ndugu zetu wengine wakiwa wakiabudu msikitini, nao wamekatishwa maisha yao. Sisi kwetu hapa pia hatupo salama, yupo mzee mmoja katika tarafa hii ya Mtinko amelazimishwa na mtoto wake kuyaaga maisha ya hapa dunaiani,” alisema mwenyekiti huyo  kwa masikitiko makubwa.
Akisisitiza, alisema kuwa kuna umuhimu mkubwa kwa viongozi wetu wa madhehebu ya dini wakatenga muda, kwanza kwa kuwakumbusha waumini wao kwamba kuuawa binadamu mwenzake ni dhambi mbele ya Mungu.
“Pia maombi au sala maalum zifanyike ili shetani ambaye amewaingia baadhi ya Watanzania wenzetu kuanza kazi haramu ya kuuawa watu wasio na batia, aweze kushindwa,” alisema Hanje.
Aidha, mwenyekiti huyo amewaomba wananchi kutoa taarifa mapema Polisi endapo watabaini dalili za viashiria vya viteno vya mauaji ya watu wasio na hatia ili viweze kudhibitiwa.
“Vile vile niombe Jeshi la Polisi kuwasaka wale wote wanaojihusisha na vitendo vya mauaji ya watu wasio na hatia na kuwafikisha mahakamani sheria iweze kuchukua mkondo wake. Vivyo hivyo kwa waganga wanaotoa ramli chonganishi,” alisema Hanje.
Katika hatua nyingine, Hanje amewataka viongozi wa dini wasijihusishe na masuala ya uhaba wa sukari na kazi hiyo waiachie serikali ya awamu ya tano ambayo tayari imeishachukua hatua la kumaliza tatizo hilo.
“Wafanyabiashara wa sukari, nawaombeni mmuogope Mungu, acheni kuficha sukari … mtawaomiza Watanzania wenzenu. Kadhalika acheni kuuza sukari kwa bei ya juu, uzeni kwa bei elekezi iliyotolewa na serikali yenu. Hii bidhaa ni muhimu kwa maisha ya kila Mtanzania, muungeni mkono rais wetu kwa kuhakikisha sukari inapatikana wakati wote, na kwa bei iliyotolewa na serikali,” alisema.
Wakati huo huo,Tamari Aron Mbogho (10), muda mfupi kabla ya kuagwa mama yake Dk.Sofia, alimwimbia wimbo mama yake kwa kiingereza na kuutafsiri kwa kishwahili,kitendo hicho kilipelekea baadhi ya viongozi wa dini na waombolezaji kwa ujumla, kububujikwa machozi na wengi kushindwa kujizuia na kulia kwa nguvu.