JUMLA ya makubaliano 11 ya ushirikiano katika sekta mbalimbali,
itasainiwa kati ya Serikali ya Tanzania na Morocco wakati wa ziara ya
Mfalme wa Morroco, Mohamed VI.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alibainisha hayo jana
wakati akizungumza na waandishi kuhusu ziara ya Mfalme huyo, anayekuja
nchini kesho kwa ziara ya kiserikali.
Makonda alisema ziara ya kiongozi huyo, itakiwa na manufaa makubwa
kwa nchi, kwani akiwa na mwenyeji wake, Rais John Magufuli watasaini
makubaliano 11 ya ushirikiano katika sekta za kilimo, gesi, mafuta, Reli
ya Liganga na Mchuchuma na sekta ya utalii.
Mohamed VI anatarajiwa kufanya ziara ya kiserikali ya siku tano,
ambayo ina lengo la kuimarisha uhusiano kati ya Morroco na Tanzania.
Makonda alitoa mwito kwa wakazi wa Dar es Salaam, kujitokeza kwa wingi
kumpokea mgeni huyo atakayeambatana na wageni zaidi ya 1,000 na ndege
kubwa sita.
Alisema ujio huo utawanufaisha wafanyabiashara wa hoteli ambazo
zitatumika kuwahifadhi wageni hao. Aidha Makonda aliwaomba radhi wakazi
wa jiji hilo kwa usumbufu watakaopata, kutokana na barabara kadhaa
kufungwa siku hiyo ili kuruhusu misafara ya viongozi hao wakuu.
Juzi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Balozi Dk Augustine Mahiga , alisema ziara rasmi ya Mfalme Mohammed VI
wa Morocco hapa nchini, itaanza Jumapili (kesho).
Baada ya ziara rasmi, atakuwa na likizo na atatembelea sehemu
mbalimbali kama matembezi binafsi. Pia, atatembelea Zanzibar na kukutana
na Rais Ali Mohamed Shein na pia atatembelea Mamlaka ya Hifadhi ya
Ngorongoro (NCCA) kwa ajili ya kujionea vivutio vya utalii vilivyopo
nchini.
Hali kadhalika, mfalme huyo pia atatembelea taasisi za kidini, ambapo
ataweka jiwe la msingi la ujenzi wa msikiti wa Kinondoni, na kukutana
na viongozi wa dini ya Kiislamu na ataswali sala ya Ijumaa huko
Zanzibar.



0 comments :
Post a Comment