Kamati
ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) leo imekifungia
kipindi cha ‘Take One’ kinachorushwa na kituo cha runinga cha Clouds tv,
kwa kipindi cha miezi mitatu mfululizo kuanzia leo.
Makamu
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Joseph Mapunda amesema kuwa kipindi hicho
kimefungiwa baada ya kilichorushwa Agosti 9, 2016 kukiuka kanuni za
huduma za utangazaji (Maudhui).
Kutokana
na mtangazaji wake Zamaradi Mketema kufanya mahojiano na Gift Stanford
‘Gigy Money’ ambayo kamati hiyo imeyatathimini na kubaini kuwa yalikiuka
maadili na kanuni za utangazaji.
Mapunda
amesema, kipindi hicho pia kimeingilia masuala binafsi ya watu kwa
kuyaweka wazi na kutaja majina bila ya ridhaa yao. Kipindi hicho pia
kimedaiwa kuwa na mwelekeo wa kuhamasisha vijana kufanya biashara ya
ngono ili kujipatia fedha.
Pia amesema kamati hiyo imetoa onyo kwa kituo cha Clouds Television kwa kukiuka Kanuni za Huduma za Utangazaji (maudhui) 2005.
“Clouds
Television inapewa onyo kali kwa kukiuka kanuni za Huduma za Utangazaji
(Maudhui) 2005 Na. 5 (c,d,e,f,) na 9 (1), 14 (1) na 15 (c),” amesema na
kuongeza.
“Kipindi
cha Take One kinafungiwa kwa kipindi cha miezi mitatu kuanzia leo,
katika muda huo wa kufungiwa, Clouds inatakiwa kukitathimini kwa lengo
la kupata njia bora ya kukiendesha na kupeleka mapendekezo TCRA kwa
ajili ya kuridhia kabla ya kipindi hicho kufunguliwa,” amesema.
Aidha, Mapunda amesema kabla ya kamati hiyo kutoa maamuzi hayo, uongozi wa Clouds Television ulitoa utetezi wake.
Hata
hivyo, Mapunda amesema haki ya kukata rufaa dhidi ya uamuzi huo katika
Baraza la Ushindani wa Haki na Biashara uko wazi ndani ya siku 30
kuanzia leo.


0 comments :
Post a Comment