KOCHA Msaidizi wa Klabu Bingwa ya 
Afrika Mashariki na Kati Azam FC, Idd Nassor Cheche, amesema kuwa 
wanakipanga vema kikosi hicho kuelekea mchezo ujao dhidi ya Simba ili 
kuifunga tena na kulinda heshima waliyoiweka Zanzibar hivi karibuni 
walipoichapa na kutwaa ubingwa wa Kombe la Mapinduzi.
Azam FC inaendelea na maandalizi 
makali chini ya Kocha Mkuu, Aristica Cioaba na wasaidizi wake, Cheche na
 Kocha wa Makipa, Idd Abubakar, ambao wamekuwa wakikiweka vema kikosi 
hicho kuelekea mchezo huo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) 
utakapofanyika Uwanja wa Uhuru Jumamosi Ijayo saa 10.00 jioni.
Cheche mara baada ya mazoezi ya leo asubuhi, ameuambia mtandao rasmi wa klabu www.azamfc.co.tz
 kuwa vijana wake wanamorali kubwa kuelekea mchezo huo na wanaomba na 
kutamani Jumamosi hata ingekuwa kesho kutokana na namna walivyojiandaa 
vilivyo.
“Hivi sasa tunaendelea na 
maandalizi vijana wako kambini na mazoezi wanafanya kwa nguvu zote kwa 
kufuata maelekezo na makosa waliyofanya katika mechi zetu zilizopita 
tunaendelea kuyafanyia kazi ili tubadilike kidogo na kufanya vema zaidi 
katika mchezo huo.
“Hali ya vijana wangu ipo vizuri, 
wanamorali kubwa na wanajitihada ya kufanya kitu, sisi tunatarajia 
mchezo utakuwa mkali na wa ushindani lakini vijana wetu watapambana hadi
 tone la mwisho la damu na kuhakikisha tunalinda heshima tuliyoiweka 
Zanzibar,” alisema.
Nafasi ya Azam kutwaa ubingwa
Akizungumzia muelekeo wa ligi 
ulivyo na nafasi waliyopo kama bado wako kwenye mbio za ubingwa, Cheche 
alisema wataendelea kupambana hadi mwisho katika kusaka taji la ligi 
hiyo.
“Bado tunamechi nyingi hatuwezi 
kusema labda tukate tamaa, lolote linaweza kutokea kwa hiyo sisi 
tunataka kuhakikisha mechi zetu zote zilizobakia tunashinda, kama 
aliyetangulia atateleza basi sisi tutachukua nafasi yake,” alisema.
Timu hizo zinakutana wakati Azam 
FC ikiwa nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi ikibeba pointi 31 
ikizidiwa pointi 14 na Simba iliyojikusanyia 45 kileleni, Yanga ni ya 
pili ikiwa nazo 43 huku Kagera Sugar iliyocheza mchezo mmoja zaidi 
ikikamata ya tatu ikiwa nazo 34

0 comments :
Post a Comment