Majeruhi wanane urais CCM

Dar es Salaam. Wakati mchakato wa kumtafuta mgombea wa urais kwa tiketi ya CCM ukiwa umekamilika, ni dhahiri kwamba baadhi ya vigogo waliokuwa na matumaini makubwa ya kuukwaa, sasa wanaugulia maumivu huku wengine wakiwa wameshautangazia umma kutoendelea na ubunge.
Licha ya kuwa siasa ni pata potea, kwa wanasiasa vijana huenda mchakato huo ukawa ni mwanzo wa safari ya kuelekea kwenye kilele cha mafanikio na kwa baadhi ya vigogo huenda ukawa ndiyo mwanzo wa kuelekea kustaafu siasa.
Edward Lowassa, Frederick Sumaye, Dk Mohammed Gharib Bilal, Stephen Wasira, Mizengo Pinda, Samuel Sitta na Profesa Mark Mwandosya ni makada waliojitokeza kujaribu bahati yao ya kuteuliwa kugombea urais, lakini ni dhahiri kuwa sasa watakuwa wanaanza kujiwekea mazingira ya kuachana na siasa.
Wote hawakumudu kuingia kwenye orodha ya wagombea watano waliopelekwa kwenye Halmashauri Kuu kwa ajili ya kuchujwa hadi kubakia watatu ambao hupelekwa kwenye Mkutano Mkuu kwa ajili ya kumpata mgombea urais wa CCM.
Kwa mujibu wa utaratibu wa CCM wa kumuachia mteule agombee kwa vipindi viwili iwapo anashinda uchaguzi wa Rais, makada hao sasa watalazimika kusubiri hadi mwaka 2025 ili kujaribu tena bahati yao, jambo ambalo linaonekana halitakuwa rahisi.
“Nyakati za kisiasa zinabadilika haraka sana. Miaka 10 ijayo siyo mchezo,” alisema Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria Tanzania (OUT), Hamad Salim alipohojiwa na Mwananchi kuhusu mustakabali wa makada waliokosa nafasi ya kupeperusha bendera ya CCM kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25.
“Kwa kipindi hicho, mambo mengi yatabadilika, wanasiasa waliogombea kipindi hiki hawawezi kuwa kwenye umaarufu wa sasa, wanaweza kupanda chati au kushuka.
 “Pia, kuna suala la umri wazee kama Dk Bilal au Sumaye miaka 10 ijayo kupanda jukwaani na kushuka mara kwa mara itakuwa shida kidogo. Wanasiasa wengi waliokuwamo kwenye kinyang’anyiro hicho ni wazee na ule siyo umri wa kushinda majukwaani.”
Licha ya sifa za mgombea kutozungumzia umri wa juu bali wa chini ambao ni kuanzia miaka 40, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Richard Mbunda alishauri baadhi ya vigogo walioshindwa kupumzika kupisha damu changa za mabadiliko.
Alisema: “Siasa nchini hazitabiriki na ni za kipekee kwani unaweza ukawa maarufu usichagulike na siku zinavyokwenda ukapoteza umaarufu huo.
“Kwa hali ya sasa, Bilal, Pinda, Lowassa, Sitta tayari walishakamata nafasi za juu nchini na umri wao umeshasogea. Bila shaka ni muda muafaka kupisha wengine… wameshaitumikia nchi vya kutosha na wana marupurupu ya kutosha baada ya kustaafu. Ni bora wawaachie vijana walete mabadiliko,” alisema Mbunda.
Alisema makada hao ni washauri wazuri iwapo wataachana na siasa za kushindana. Alisema hata kwa wale ambao umri unawaruhusu, haitakuwa vizuri kuwapa vyeo vidogo kama vya ubalozi na kwa maana hiyo alisema safari yao kisiasa, imefikia ukingoni.
Mchakato huo wa urais wa CCM ulitawaliwa na jina la Lowassa, ambaye alikuwa akipewa nafasi kubwa ya kuteuliwa baada ya harakati zake za kusaka wadhamini kuhudhuriwa na maelfu ya watu kuthibitisha kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuwa chama hicho kingechagua mtu anayekubalika ndani na nje ya CCM.
Lakini hakumudu kuingia tano bora na hivyo kuacha mgogoro mkubwa uliosababisha wajumbe wa Halmashauri Kuu kumuimbia Kikwete wimbo ulioonyesha kuwa wana imani na mbunge huyo wa Monduli.
Majeraha kwa waziri huyo mkuu wa zamani, pia yanaonekana kwenye kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na Kingunge Ngombale Mwiru ambaye alikuwa mstari wa mbele kumnadi na ambaye ameeleza wazi kuwa viongozi wa CCM walikula njama kumuengua.
Lowassa (62) pia alijitosa kwenye mchakato huo mwaka 1995 alipokwenda kuchukua fomu pamoja na Kikwete, lakini jina lake likaenguliwa.
Dk Bilal
Kada mwingine anayeonekana kuachwa akiwa na majeraha makubwa ni Dk Bilal, ambaye ni Makamu wa Rais. Bilal amepoteza nafasi ya kuendelea kushika nafasi hiyo baada ya mteule wa CCM, Dk John Magufuli kumpendekeza Samia Salim Suluhu kuwa mgombea mwenza. Kwa makamu wa Rais kutoingia tano Bora ni pigo kubwa.
Dk Gharib (70) aligombea urais wa Zanzibar mwaka mwaka 2010 na kushindwa, lakini CCM ikamteua kuwa mgombea mwenza wa Kikwete baada ya Dk Mohamed Shein kuteuliwa kugombea urais wa Zanzibar. Atakuwa akiuguza majeraha kwa kuwa mtu wa kwanza kushikilia nafasi hiyo kwa kipindi kimoja tangu siasa za ushindani zirejeshwe nchini.
Membe
Kundi lililoachwa na majeraha pia linamjumuisha Membe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, ambaye ameaga sehemu mbalimbali alizokuwa zikimhusu kutokana na kazi yake ya kisiasa na hasa jimboni kwake ambako tayari Katibu Mwenezi wa CCM, Nape Nnauye ameshachukua fomu.
Membe (62) amefanya wizara hiyo kwa takriban miaka minane na alikuwa mmoja wa makada waliokuwa wanapewa nafasi kubwa. Alipenya kwenye tano bora, lakini akashindwa vibaya kwenye kura za wajumbe wa Halmashauri Kuu na sasa atakuwa akitafakari upya hatma yake kisiasa.

Pinda
Waziri Mkuu, Pinda naye ameachwa na majeraha. Ameingia kwenye orodha ya watu walioshika cheo hicho na ambao wamejaribu kuwania urais na kuenguliwa mapema.
Machungu ya kuenguliwa Pinda (67) pia yanatokana na ukweli kuwa alikuwa mtendaji mkuu wa Serikali na hivyo ilikuwa rahisi kushauriwa kutojiingiza kwenye mchakato kama hakuwa na nafasi hata ya kuingia tano bora.
Mbunge huyo wa Katavi ameshatangaza kuachia jimbo hilo na baada ya matokeo hayo, mustakabali wake utategemea busara ya viongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.
Profesa Mwandosya
Mchakato huo pia umeacha jeraha katika jaribio la pili la Profesa Mwandosya, ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), la kuwania urais baada ya mwaka 2005 kushika nafasi ya pili nyuma ya Kikwete aliyeongoza na Dk Salim Ahmed Salim.
Profesa Mwandosya, kama baadhi ya makada walioenguliwa, ameshatangaza kutogombea ubunge Jimbo la Rungwe Mashariki, hali ambayo imesafisha njia ya kuelekea kustaafu siasa baada ya kushindwa kwenye mbio za urais.
Sitta
Spika huyo wa Bunge la Tisa na pia Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, anaingia kwenye orodha ya majeruhi wa mchakato wa urais wa CCM baada ya kujiandaa kwa muda mrefu kuwania nafasi hiyo.
Sitta alisema bayana wakati alipochaguliwa kuongoza chombo hicho cha kihistoria cha kuandika Katiba kuwa atatumia uspika wake kutengeneza mazingira ya kuteuliwa na CCM kugombea urais.
Lakini naye hakupenya hata kwenye tano bora na inaelekea hatua inayofuata ni kwenda Tabora kutetea jimbo lake.
Akiwa na umri wa miaka 73, mwanasiasa huyo mkongwe sasa hana nafasi ya kugombea tena urais baada ya miaka 10 atakapokuwa na umri wa zaidi ya miaka 80.
Sumaye
Waziri Mkuu huyo wa Serikali ya Awamu ya Tatu, atakuwa akiuguza majeraha ya kupoteza nafasi ya kuteuliwa kwa mara ya pili baada ya jaribio lake la kwanza mwaka 2005 kugonga mwamba.
Alishaachana na siasa za majimbo tangu mwaka 2005 baada ya kukosa urais na akiwa na umri wa miaka 65, haiyumkini kuingia tena kwenye mbio za urais mwaka 2025.
Wasira
Waziri huyo wa Kilimo, Chakula na Ushirika, alitangaza awali kuwa asingegombea ubunge wa Bunda, lakini akabadilisha uamuzi huo licha ya kuingia kwenye mbio za urais. Wasira, ambaye mwaka huu ametimiza miaka 70, atakuwa akiwania kurejea bungeni akipambana na mwanasiasa kijana ndani ya CCM, Esther Bulaya.
 “Ni wazi kwa waliokuwa na matumaini makubwa ya kushinda ni pigo sana kuangushwa. Hata matamshi yao yalikuwa wazi kuwa walikuwa na uhakika hata walidiriki kusema ‘jina langu halitakatwa’ na mbio zao za kutafuta wadhamini zilikuwa ni za kishindo,” alisema Profesa Gaudence Mpangala, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Ruaha (Ruco).
Profesa huyo wa masuala ya siasa na utawala, alisema kwa hali ya kawaida wagombea hao wameathirika kisaikolojia, hivyo hata wale waliokuwa wametangaza kutogombea wanaweza kubadili msimamo na kurudi kutetea majimbo yao.

“Magufuli akipata urais anaweza kuwafikiria hata uwaziri na iwapo upinzani watashinda, hali yao kisiasa ndiyo basi tena. Siasa siyo kazi ya kudumu, bali ni ya muda tu wa kuwatumikia wananchi ukimalizika, unastaafu.”
MWANANCHI
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment