MOTO
wa rais Dk. Magufuli wa utumbuaji wa majipu umepiga hodi hadi kwenye
madhehebu ya dini Mkoani Singida, baada ya Katibu BAKWATA wilaya ya
Singida Vijijini, Salum Abrahaman Masaka, kutumbuliwa jipu/kusimamishwa
kazi kwa nuda usiojulikana kutokana na tuhuma ya ubadhirifu wa shilingi
640,000 mali ya BAKWATA.
Akizungumza na Modewjiblog
ofisini kwake, Katibu wa Baraza kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) mkoa
wa Singida, Alhaji Burhan Mlau, alisema Salum amesimamishwa kazi
kuanzia April 19 mwaka huu.
Alisema maamuzi hayo mazito na magumu, yametolewa na kikao halali cha halmashauri ya wilaya ya Singida vijijini.
“Baadhi
ya tuhuma zinazomkabili Salum ni pamoja na kusababisha hasara ya
shilingi 640,000 ambayo ni amana na waislamu wa Singida
vijijini,kudanganya Jumuiya ya akina mama kwamba angewapa gunia moja la
mahindi na amekuwa akikusanya mapato ya usajili wa ndoa na
hajaziwasilishi kwenye mamlaka husika”,alisema.
Akifafanua,
Alhaj Mlau alisema kutokana na tuhuma ambazo zinaendelea kufanyiwa
uchunguzi, imewalazimu wamsimamishe kazi, ili kupisha uchunguzi huo hadi
hapo uamuzi mwingine utakapofanyika.
“kwa
kifupi Salum amesimamishwa kazi baada ya halmashauri ya wilaya ya
Singida vijijini kukosa imani na utendaji wake wa kazi”, alisema.
Katibu huyo,alisema kwa sasa nafasi hiyo amekaimishwa Said Alli Mang’ola.
Wakati
huo huo, Alhaji Mlau, ametoa wito kwa watendaji wa BAKWATA mkoani
Singinda wawe waadilifu, waaminifu na kutunza vizuri mali ya waumini.
“Nikumbushe
tu kwamba dini ya Kiislamu, ni dini ya kweli, imani, utulivu na haina
kabisa nafasi ya viongozi wenye tama ya kujinufaisha binafsi na mali ya
Waumini”,alisisitiza.
Hivi
karibuni Askofu wa Kanisa la Pentekoste (FPCT) Jimbo la Singida Amos
Maghasi, akifungua mafunzo ya viongozi wanawake wa Kanisa hilo, alidai
kuwa majipu hayapo serikalini tu, yapo hadi ndani kwenye madhehebu ya
dini.
Imeandaliwa na Nathaniel Limu, Singida


0 comments :
Post a Comment