Nkupamah media:
Kamanda wa Polisi kanda hiyo, Simon Sirro.
Wiki iliyopita, jumuiya hiyo ilipanga kufanya maandamano ya amani
ya kuunga mkono maazimio ya kikao cha Baraza Kuu Taifa, kutoshiriki
marudio ya uchaguzi wa Zanzibar uliopangwa kufanyika Machi 20, mwaka
huu, lakini Jeshi la Polisi liliyazuia.
Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Saverena Mwijage, jana alilieleza
Nipashe kuwa, Kamanda wa Polisi kanda hiyo, Simon Sirro, aliwaeleza
sababu za kuzuia maandamano hayo kuwa uchaguzi huo umetangazwa kufanyika
Zanzibar kwa maana ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec) na si Tanzania
Bara.
Alisema sababu nyingine ni kuhatarisha usalama wa raia na mali zao kutokana na siku waliyoomba kufanya maandamano ni ya kazi.
Alisema pia waliambiwa waandike barua ya kuomba kibali cha kumuona
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, ili kumueleza walichokusudia.
“Barua hiyo tulijibiwa Ijumaa wiki iliyopita siku moja baada ya
kupeleka barua ya kuomba kibali na hata hivyo, hatukuridhishwa kabisa na
sababu za kuzuia maandamano yetu kwani tunalenga kufanya kwa amani,”
alisema.
Mwijage alisema kutokana na Zec kuendelea kutoa msimamo wake wa
marudio ya uchaguzi na kudai barua aliyoandika aliyekuwa mgombea wao,
Maalim Seif Sharif Hamad, kuwa siyo halali na hajajiondoa kwenye
uchaguzi huo, walilazimika kuandika barua nyingine ya kuomba maandamano
jana.
“Kwa sababu Zec bado wanaendelea na msimamo wao wa kurudia kwa
uchaguzi na kumlazimisha mgombea wetu kuwa ni halali wakati alishaandika
barua na sisi tunapinga vikali na dunia itambue jambo hili batili,
kupitia maandamano haya ya amani,” alisisitiza.
Alisema jana waliandika tena barua na kuituma kwa Jeshi la Polisi kuomba kibali cha kufanya maandamano ya amani.
“Kwa sababu walishasema maandamano yetu tuliomba siku ya kazi, basi
tumeomba watupangie siku ambayo tutayafanya bila kubughudhi watu,”
alisema.
Maandamano hayo yalipangwa kuanzia katika Makao Makuu ya CUF
Buguruni na kupita barabara ya Uhuru, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es
Salaam, Karume, Kariakoo, Mnazi Mmoja, Central Polisi, barabara ya
Sokoine, Bandarini, Mahakama Kuu na Ardhi hadi Ofisi ya Makamu wa Rais.


0 comments :
Post a Comment