Zinaweza kuwa taarifa za kuwashtukiza mashabiki wengi wa Manchester City lakini haina jinsi kuona kiungo mshambualiaji wa klabu hiyo, Kevin De Bruyne akiwa nje ya dimba wakati timu yake ikipambana na Barcelona katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, Oktoba, 19 mwaka huu.
Jambo hilo linakuja baada ya kutolewa taarifa ya De Bruyne alipata majeraha ya misuli ya paja katika mchezo wa Jumamosi dhidi ya Swansea hivyo atakuwa nje ya uwanja kwa muda wa wiki nne.
De Bruyne alitolewa katika dakika ya 81 ya mchezo huo ambao Man City ilipata ushindi wa goli 3-1, na kwenda kufanyiwa vipimo ambavyo vimeonyesha kuwa alipata majeraha hivyo anatakiwa kuwa nje ya uwanja ili kutibu majeraha yake.
Michezo mingine ambayo De Bruyne ataikosa ni mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya UEFA dhidi ya Celtic unaotaraji kupigwa Jumatano na michezo miwili ya Ligi Kuu ya Uingereza dhidi ya Tottenham na Everton.