Tume
ya Haki za Binadamu na Utawala Bora leo imeadhimisha miaka 50 ya
kuzaliwa kwake jijini Dar es Salaam, kwa kutoa tuzo za uwajibikaji na
utawala bora kwa familia ya muasisi wa Taifa hili na aliyekuwa rais wa
awamu ya kwanza Hayati Julias Kambarage Nyerere na Rais Mstaafu wa awamu
ya pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Alhaji Ally Hassan Mwinyi.
Mkurugenzi
wa Haki za Binadamu na Utawala Bora, Bahame Nyanduga, wakati Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,
Angellah Kairuki akiikabidhi tuzo ya Mwl. Nyerere kwa mjukuu wake
Moringe Nyerere, amesema tume hiyo itaendelea kumkumbuka Baba wa Taifa
kwa kuwa ndiyo muasisi wa tume hiyo, vilevile aliacha msingi mzuri wa
utawala bora na haki za binadamu nchini.
“Tuzo
hii imetolewa kwa familia ya Mwl. Nyerere kutokana na kazi nzuri
aliyofanya ya kukuza haki za binadamu na utawala bora nchini, pia ndiye
muasisi wa tume hii,” amesema.
Nyanduga
amesema kuwa, tuzo ya pili imetolewa kwa rais mstaafu Mwinyi kutokana
na mchango wake katika kusimamia misingi ya haki za binadamu na utawala
bora enzi za utawala wake.
“Rais
Mwinyi aliwajibika, alijituma, na kuhakikisha watumishi wa umma
wanatekeleza majukumu yao kwa misingi ya utawala bora kwa kuzingatia
matakwa ya sheria, katiba na kanuni,” amesema.


0 comments :
Post a Comment