Utafiti mpya wa ugonjwa wa Virusi vya Ukimwi (VVU), unatarajiwa kuleta faraja kwa wenzi, ambapo mmoja anaishi na virusi hivyo na mwingine akiwa hana.
Faraja
hiyo inahusisha kufanya tendo la ndoa bila kutumia kinga na hivyo
kupata watoto bila kusababisha maambukizo yoyote mapya baada ya unywaji
wa dawa.
Ugunduzi
wa dawa hiyo mseto ya kimiminika ijulikanayo kama PrEP, tayari
imetumiwa na wanaume mashoga nchini Uingereza na Marekani.
Dawa
hiyo huweza kuondoa hatari ya kuambukizwa hadi asilimia sifuri,
itaondoa changamoto iliyokuwapo katika njia namba moja ya kujikinga na
virusi, yaani kutumia kondom wakati wa kufanya tendo la ndoa.
Matumizi
ya kondom yalimaanisha kuwa wenzi wa aina hiyo hawawezi kupata watoto
bila uwezekano wa kuhatarisha mwenzi ambaye hana VVU.
Kwa sababu hiyo, mamlaka nchini Kenya zimeanzisha mradi wa kuwasaidia wenzi kuwa na familia bila kuhatarisha afya zao.
John
na mkewe Josephine, wanaoishi kaskazini mwa Nairobi ni mfano wa wenzi
wa aina hiyo, ambapo Josephine anaishi na VVU wakati John hana
maambukizo hayo.
Mume huyu anasema kuwa hali kama hiyo inaweza kuwa ngumu na anawajua wenzi ambao wameshatengana kwa sababu hiyo.
Kuna wenzi 260,000 nchini Kenya, ambako mmoja anaishi kwa VVU huku mwenzake akiwa hana.
Wenzi
wa aina hiyo wanaojulikana kitaalamu kama serodiscordant, wanachukua
asilimia 44 ya mambukizo mapya ya VVU katika taifa hilo. Pamoja na
asilimia hiyo wamezaa watoto.
“Lakini
nia ya kupata watoto kwa wenzi wa aina hii bado huwa na nguvu mno
–utafiti mmoja wa hivi karibuni kwa wenzi wa serodiscordant umeonesha
asilimia 17 ya wanawake walipata mimba.
“Kwa sasa majaribio mapya ya dawa yametoa mwanga wa matumaini na faraja kwa wenzi wa aina hii,” anasema John.
Imebainika
kwamba njia mpya ya kutumia dawa za kukabiliana na VVU, ambazo kwa
kawaida hupewa watu wanaoishi na virusi hivyo, inaweza kutumika kwa
wenzi wa aina hiyo kujaribu kuzaa watoto wasio na VVU bila pia
kumwambukiza mwezi asiye na virusi hivyo.
Dk.
Nelly Mugo kutoka Taasisi ya Utafiti wa Tiba ya Kenya na timu ya
wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Washington cha nchini Marekani kwa
pamoja wanaendesha majaribio hayo.
Majaribio hayo yalihusisha wenzi 4,700, ambao mmoja ana VVU na mwingine hana maambukizo.
Katika majaribio hayo, mtu ambaye hakuambukizwa VVU alikunywa PrEP katika kipindi cha miezi 36.
“Tulibaini kwamba kuwa na dawa katika mfumo wako mwilini kulipunguza kiwango cha maambukizo kwa zaidi ya asilimia 90.
“Lakini
pia iwapo mwenzi mwenye VVU pia alichukua dawa za kufubaza makali ya
Ukimwi (ARVs), uambukizo wa VVU ulipunguzwa hadi asilimia sifuri au
karibu na sifuri,” alisema.
Katika
baadhi ya jamii shinikizo la kijamii la kutaka kuwa na watoto linaweza
kuwa kubwa huku familia zisizo na watoto mara nyingi zikipata shida
kueleza kwanini hazijazaa.
Katika
utafiti wa karibuni, wenzi walieleza kwamba walijisikia kutokuwa na la
kufanya na wako katika hatari ya kupata VVU iwapo watajaribu kupata
mimba.
Lakini
katika mradi wa sasa, wenzi wasioambukizwa walipata faraja baada ya
kubakia salama bila kuambukizwa walipofanya tendo la ndoa bila kinga,
hali iliyosababisha imani kwa dawa hiyo kuwa na uwezo wa kuwalinda.
Dk. Mugo anasema:
“Hisia za kawaida zilizozoeleka kwa kuzaa watoto ni pamoja na kutimiza
matarajio ya wenzi husika ya ukubwa wa familia waitakayo, kupata watoto
wao wenyewe wa kuwazaa na kuendeleza uhusiano imara na mara nyingi
muhimu zaidi ikiwa ni kukabiliana na shinikizo la nje kutoka kwa jamii” alisema.
VVU
haitibiki, kwa sababu mara inapoingia katika mwili, hujificha katika
mahali ambapo ni vigumu kupafikia, na kusababisha hodhi, hali
inayomanisha kwamba kamwe haiwezi kuondolewa kutoka humo hodhini.
Nadharia iliyo nyuma ya PrEP ni kwamba kuchukua dawa za ARVs kabla ya kuambukizwa kunamaanisha tayari zipo ndani ya mwili.
Lakini
watafiti wameonesha kuwa iwapo mtu asiyeambukizwa tayari atakuwa na
dawa za PrEP katika mifumo yao ya mwili wakati virusi vinapoingia katika
miili yao hiyo huuawa.
Hili linamaanisha kuwa virusi huwa havina nafasi ya kujificha katika hodhi, na hivyo ni vigumu kwa mtu kuambukizwa.
“PrEP ni kitu kizuri kinachoweza kuwafaa wenzi hawa,” anasema Dk. Mugo, kwa sababu inaweza kutatua kile alichokiita ‘hali tete ya ufarakano.
“Wakati unapobaini mwenzi wako ana VVU husababisha maumivu makubwa ya kihisia,” aliongeza. “Lakini uhusiano na hisia na mapenzi vina nguvu kuliko virusi.
“Wengi
wa wenzi hutaka kubakia pamoja, lakini wanashindwa kurejea katika hali
ya kawaida ya uhusiano wa tendo la ndoa. PrEP ina uwezo mkubwa wa
kutatua tatizo hilo,” anasema.
Jaribio
hilo lilikuwa na mafanikio kwani kufikia Septemba 2015, Shirika la Afya
Duniani (WHO) lilipendekeza kuwa watu walio katika hatari ya kupata VVU
wapatiwe PrEP kama chaguo la pili la kujikinga, kama sehemu ya uzuiaji
wa maambukizo.



0 comments :
Post a Comment