Katibu 
mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon Ijumaa (22.04.2016) amemuwekea 
mbinyo zaidi kiongozi wa waasi nchini Sudan kusini Riek Machar kurejea 
mjini Juba "bila kuchelewa" na kuanza kazi katika serikali ya mpito.
Machar 
alitarajiwa kurejea katika mji mkuu siku ya Jumatatu, kwa mujibu wa 
makubaliano ya kisiasa yenye lengo la kumaliza vita vya miaka miwili, 
lakini tofauti kuhusiana na mipango ya kiusalama mjini Juba 
inachelewesha kurejea kwake.
Ban 
amesema serikali ya rais Salva Kiir imekubali pendekezo la muafaka 
kuhusiana na matayarisho ya kurejea kwa Machar na kusema hatua hii 
inapaswa kusaidia kuundwa kwa haraka kwa serikali mpya ya umoja wa 
kitaifa.
"Kuendelea
 na hali ya ushirikiano itakuwa muhimu wakati viongozi wa nchi hiyo 
wakianza mchakato wa kubadilisha miaka ya uharibifu uliosababishwa na 
mzozo huo kwa watu wa Sudan kusini," amesema katika taarifa.
Mateso ya watu wa Sudan kusini
Ban 
amemtaka Machar kusafiri kwenda Juba " bila masharti zaidi" hali ambayo 
inaweza kuchafua mchakato wa amani na kuendeleza hali ya mateso 
yanayowakuta watu wa Sudan kusini."(P.T)
Chini ya 
makubaliano ya amani, Machar alitakiwa kurejea tena katrika wadhifa wake
 wa makamu wa rais katika serikali mpya itakayodumu kwa muda wa miezi 30
 na kuielekeza nchi hiyo katika uchaguzi mkuu.
Kikwazo 
cha hivi sasa kinahusiana na idadi ya bunduki na vifaa vya kufyatulia 
maguruneti ambavyo vikosi vya waasi vinavyomlinda Machar vitaruhusiwa 
kuwa navyo.
Vita vya 
Sudan kusini vilianza Desemba mwaka 2013, wakati Kiir alipomshutumu 
Machar kwa kula njama za kumpindua. Mzozo huo umeweka wazi mpasuko wa 
tofauti za kikabila na umekuwa ukionesha ukiukaji mkubwa wa haki za 
binadamu, ikiwa ni pamoja na ubakaji wa makundi, uchomaji moto vijiji na
 hata ulaji nyama za watu.
Ombi la Marekani
Kwa ombi 
la Marekani, baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilikutana siku ya 
Jumatatu na kuelezea "wasi wasi wake mkubwa " kwa kushindfwa kurejea 
Machar mjini Juba.
Jumuiya 
zenye nguvu duniani, ikiwa ni pamoja na Umoja Umoja wa Afrika, Umoja wa 
Ulaya , China , Uingereza na Marekani , zimewapatia Machar na Kiir muda 
wa mwisho hadi leo Jumamosi (23.04.2016) kutatua tofauti zao.
Mamia kwa
 maelfu ya watu wameuwawa na zaidi ya watu wengine milioni mbili 
wamelazimika kuyakimbia makaazi yao tangu vita hivyo vilipozuka Desemba 
mwaka 2013.
Wasiwasi unatuwama katika hali ya kutoaminiana kuhusiana na silaha hali ambayo imechelewesha kurejea kwa Machar.
Kikosi 
cha wanajeshi waasi wapatao 1,370 tayari kimewasili mjini Juba kama 
sehemu ya makubaliano ya amani wakati majeshi ya serikali yanasema 
yameondoa wanajeshi wake wote isipokuwa wanajeshi 3,420 , kwa mujibu wa 
makubaliano. Wanajeshi wengine wote wanapaswa kubakia kiasi ya kilometa 
25 nje ya mji mkuu.
Katika 
moja kati ya kambi tatu za waasi mjini Juba, waasi wanatengana na kambi 
ya majeshi ya serikali kiasi ya mwendo wa miguu wa dakika tano na 
wanaweza kuonana na karibu iwapo kutatokea rabsha zozote.
Chanzo:DW


0 comments :
Post a Comment