Agosti, 20 China walifanya uzinduzi wa daraja refu zaidi la kioo ambalo kwa muda mfupi ambao limefunguliwa China imeonekana kupata watalii wengi wakitaka kupita katika daraja hilo lililopo katika hifadhi ya Zhangjiajie.
Lakini kwa kipindi kifupi tangu kulifungua imetoka taarifa kuwa daraja hilo limefungwa kwa muda usiojulikana na hivyo wageni waliopanga kwenda kupita darajani hapo hawataweza tena kupita.
Daraja la Kioo
Msemaji wa hifadhi ya Zhangjiajie Grand Canyon, amesema wamefikia uamuzi wa kulifunga daraja hilo kwa sababu ya idadi kubwa ya watu ambao wamekuwa wakipita tofauti na idadi iliyokadiliwa wakati wa ujenzi.
“Limezidiwa uzito na idadi ya wageni ambao wanalitumia, idadi ya watu wanaotakiwa kupita kwa siku ni 8,000 lakini sasa wanapita mara 10 zaidi ya hiyo,” alisema.
Aidha alisema kwa sasa hakuna tatizo lolote ambalo limejitokeza ila wamechukua tahadhari mapema ili kulifanyia marekebisho ambayo yatawezesha wageni ambao wanafika katika hifadhi hiyo waweze kulitumia bila kuwa na hofu ya tatizo lolote kutokea.
Daraja la Kioo
Hata hivyo tayari watu mbalimbali ambao walikuwa wakielekea katika hifadhi hiyo wameanza kuandika maneno mitandaoni ya kukasirishwa na uamuzi huo kwani tayari walikuwa wameshatumia gharama zao ili kwenda kupita katika daraja hilo.
Daraja hilo lina urefu wa mita 430, na mita 300 zikiwa eneo la katikati ya milima jambo ambalo linafanya kuvutia zaidi watu wengi kwani ukiwa katika daraja hilo unaweza kutazama pande zote kwa uzuri kutokana na kujengwa na kioo.
Daraja la Kioo